Wajumbe wa Kamati ya Majadiliano ya Libya ya 4+4 walifikia makubaliano siku ya Jumatano ya mchakato wa kumteua mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (HNEC) baada ya utekelezaji wa mchakato wa awali kukwama.
Makubaliano hayo yalifikiwa wakati wa mkutano wa saba wa kamati hiyo katika mji mkuu wa Tunisia,Tunis, kulingana na taarifa ya Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Libya (UNSMIL).
Kamati hiyo imekuwa ikishauriana kwa miezi kadhaa baada Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa Hanna Tetteh kuliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa Aprili 22 kuwa amekuwa akizungumza na wadau kadhaa wa Libya kubaini njia za kutekeleza hatua za kwanza mbili za mchakato wa Umoja wa Mataifa.
Mchakato huo, uliotangazwa Agosti 21, 2025, umejengwa katika nguzo tatu: kuwa na mfumo ambao utakubalika kitaalamu na kisiasa kwa uchaguzi wa urais na bunge, kuunganisha taasisi za kitaifa kupitia muundo wa serikali moja, na kuanzisha majadiliano ya kitaifa.
Miswada ya makubaliano
UNSMIL inasema katika mkutano wa Jumatano, ambaye mwenyekiti wake alikuwa Tetteh, washiriki walikubaliana kuhusu mchakato wa kuteua Tume ya Uchaguzi.
“Pia waliendelea na mashauriano kuhusu vipengele kadhaa vilivyobaki vya makubaliano, huku pande zote zikikubaliana kuendelea na mashauriano wiki ijayo mjini Tunis,” taarifa iliongeza.
Wakati wa mkutano wa kwanza mjini Rome Aprili 29, wajumbe wa kamati ya 4+4 walikubaliana kuunda tena Tume ya Uchaguzi na kupendekeza kuwa Mwanasheria Mkuu Al-Siddiq Al-Sour amteue mwenyekiti mpya wa tume kutoka miongoni mwa majaji wanaofahamika kwa weledi na usawa.
Hata hivyo, baadaye kamati hiyo ikatangaza katika mkutano wake wa sita mjini Tunis Julai 14 kuwa utekelezaji wa makubaliano hayo ulikwama.
Makubaliano haya ya sasa ni sehemu ya juhudi zinazoongozwa na Umoja wa Mataifa kuandaa mazingira ya uchaguzi kwa lengo la kumaliza mgawanyiko wa kisiasa nchini Libya.















