Uturuki inafanya juhudi za kuimarisha ushirikiano na kupunguza migogoro, ndani ya Uturuki yenyewe na katika ulimwengu mzima wa Kiislamu, Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan amesema.
“Tunaamini kuwa umoja una kheri; tunajitahidi kuimarisha ushirikiano na kupunguza tofauti miongoni mwetu na katika ulimwengu wa Kiislamu,” Erdogan amesema Ijumaa katika hotuba yake kwenye hafla ya Wiki ya Mawlid al-Nabi iliyofanyika Istanbul, ambayo iliadhimisha kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (SAW).
Rais Erdogan amesema ana matumaini kwamba Waislamu, “ambao kwa karne nyingi waliunda historia na kuleta utaratibu duniani,” wataungana tena “kama matofali yanavyoungana kujenga ukuta.”
Amesisitiza umuhimu wa umoja miongoni mwa Waislamu, akiwataka kutetea haki zao na kushirikiana katika kujenga amani na usalama katika eneo hilo.
“Tunapitia mapambano ya kihistoria kati ya mema na mabaya, na kwa idhini ya Mwenyezi Mungu, mema yatashinda,” Erdogan aliongeza.
Ameonya kwamba “itikadi kali, ya unyakuajo na ya kikatili inayojulikana kama Uzayuni” si tu kwamba inatishia amani ya nchi jirani, bali pia inalenga kila mtu anayesimamia maadili ya ubinadamu.
Amesema dunia inashindwa kutoa mwitikio wa kutosha dhidi ya “sera zisizo na uhalali za mtandao wa mauaji ya halaiki wa Israel, ambazo zinapuuza sheria, kanuni, maadili na mipaka.”
Rais wa Uturuki amesema serikali ya Israel “inayotumia vita” inatumia uchochezi kuyumbisha eneo zima, ikianzia kwa nchi zinazopakana nayo.















