Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio anasema serikali ya Marekani inatangaza sera ya vikwazo vya viza inayolenga baadhi ya raia wa kigeni nchini Afrika Kusini.
Sera hiyo inalenga “raia wa nchi za kigeni wanaohusika, au kuwa sehemu, ya kupitisha au kutekeleza sheria au sera zinahamasisha uchukuaji wa ardhi bila fidia, ubaguzi kwa misingi ya rangi, na uchochezi wa vurugu dhidi ya jamii za walio wachache nchini Afrika Kusini,” Rubio alisema katika taarifa siku ya Jumanne.
Uhusiano kati ya Marekani na Afrika Kusini umekuwa mbaya tangu Donald Trump aingie madarakani kwa muhula wa pili.
Balozi wa Marekani nchini Afrika Kusini alisema katika ujumbe kwenye mtandao wa X siku ya Jumatano kuwa vikwazo vya viza kwa watu kutoka Afrika Kusini “ni hatua ya kwanza tu katika hatua kadhaa zinazopangwa kutekelezwa”.
“Serikali ya Afrika Kusini haijashughulikia masuala yaliyoainishwa awali,” Waziri Rubio alidai.
Majibu ya Afrika Kusini
Serikali ya Rais Ramaphosa imekuwa ikikataa madai ya Marekani.
Agosti mwaka uliopita, Afrika Kusini ililaumu ripoti ya serikali ya Marekani inayodai kuwa wamechukua ardhi kutoka kwa wakulima wazungu, ikitaja madai hayo ya “kupotosha” na “yasiyo na msingi”.
Maafisa wa Afrika Kusini wanasema serikali inaendelea na dhamira yake ya kulinda watu kulingana na katiba na inafanya mabadiliko kuhusu ardhi kwa kuzingatia sheria kwa lengo la kuimarisha usawa.
Afrika Kusini imetaka kukabiliana na shutma hizo za Marekani huku ikisisitiza kuendeleza ushirikiano wa kibiashara na Marekani.
Marekani ni mshirika wa tatu wa kibiashara, lakini Afrika Kusini imekuwa ikiimarisha ushirikiano na mataifa yenye uchumi mkubwa duniani kama vile China na Umoja wa Ulaya.















