Guinea-Bissau yaidhinisha katiba mpya inayompa rais mamlaka zaidi

Katiba hiyo itapunguza idadi ya wabunge hadi 65 kutoka 102.

Newstimehub

Newstimehub

1 Septemba, 2026

ba8adf13 9d7a 4d5b 90d7 8aece8d5c9b2 1788287533183

Guinea-Bissau imeidhinisha katiba mpya kupitia kura ya maamuzi, matokeo ya awali yameonesha siku ya Jumanne, yanayompa rais mamlaka zaidi na kubadilisha sheria za uchaguzi kabla ya uchaguzi wa urais uliopangwa kufanyika mwezi Disemba.

Nchi hiyo ya Afrika Magharibi inayoongozwa na jeshi ilipiga kura siku ya Jumapili kuhusu mabadiliko ambayo yatampa rais uwezo wa kumteua waziri mkuu na baraza la mawaziri na pia kuwatimua, kuunda na kubadilisha wizara pamoja na kuvunja bunge pale panapokuwa na tatizo la kisiasa.

Chini ya katiba ya sasa, Bunge la Guinea-Bissau linamtaja waziri mkuu ambaye anaunda baraza la mawaziri.

Matokeo hayo yanaipa serikali ya kijeshi uwezo wa kupanga upya mfumo wa kisiasa wa Guinea-Bissau kabla ya uchaguzi wa urais, lakini chama kikuu cha upinzani kimesusia uchaguzi huo.

Katiba hiyo mpya imeidhinishwa kwa 70% za kura na 30% walipinga, kulingana na matokeo ya awali yaliyotangazwa na Tume ya Uchaguzi. Pia ilisema kuwa watu 544,060 walipiga kura, ikiwa ni karibu 60% ya wapiga kura waliosajiliwa.

Katiba hiyo itapunguza idadi ya wabunge hadi 65 kutoka 102 na maeneo bunge kutoka 29 hadi 12.

Inahitaji wagombea urais kuwa wameishi Guinea-Bissau miaka mitano kabla ya uchaguzi.