Shirika la Msalaba Mwekundu limeeleza wasiwasi wake baada ya wahudumu sita waliokuwa wakisaidia kukabiliana na mlipuko wa Ebola kujeruhiwa wiki iliopita katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
“Mashambulizi kwa wahudumu wa kujitolea na wanaotoa misaada siyo sahihi,” Mashirika ya Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu yalisema katika taarifa siku ya Jumatatu, pamoja na Mashirika ya Msalaba Mwekundu ya DRC na Uganda.
Taarifa hiyo inasema kuwa Agosti 17, msafara wa Shirika la Msalaba Mwekundu la Uganda uliokuwa unasaidia katika kukabiliana na Ebola ulishambuliwa mkoa wa Ituri nchini DRC – kwenye mlipuko – huku mtu mmoja akishambuliwa, na ambulensi mbili kushambuliwa kwa mawe na kuharibiwa.
Siku iliyofuata, wahudumu wawili wa kujitolea walishambuliwa wakijaribu kuzika watu katika mkoa wa Haut-Uele. Walisafirishwa kwa ajili ya matibabu, ambapo magari mawili yaliharibiwa.
Vifaa vya matibabu viliharibiwa
Alafu siku ya Jumatano, eneo la Beni,mkoa wa Kivu Kaskazini, wahudumu watatu “walishambuliwa na kujeruhiwa”, huku vifaa vinavyotumika katika kukabiliana na Ebola vikiharibiwa.
Taarifa hiyo inasema mashambulizi hayo yanadhihirisha hatari ambayo wafanyakazi wa mashirika ya misaada wanakabiliana nayo wanapojaribu kutibu ugonjwa huo.
“Heshima kwa wafanyakazi wa mashirika ya misaada ni muhimu sana kuhakikisha kuwa watu walioathirika na ugonjwa huo na matatizo mengine wanapata msaada unaohitajika kwa haraka,” ilisema.















