Qatar inasema kuwa inataka utekelezaji kamili wa mpango wa makubaliano ya kusitishwa mapigano licha ya “ukaidi” wa Israel.
Msemaji wa wizara ya mambo ya nje Majed al Ansari aliwaambia waandishi wa habari siku ya Jumanne kuwa Qatar inasisitiza msimamo wake wa kuendelezwa juhudi za utekelezaji kamili wa mpango wa kusitishwa mapigano wa Gaza.
“Tunachotaka ni kuwa pande zote mbili zilizokubaliana na mpango wa Gaza kutekeleza yaliyokubaliwa kikamilifu,” alisema.
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amekataa mpango wa vipengele 15 vya kusitisha mapigano Gaza na kusisitiza kuwa Hamas isalimishe silaha kwanza, licha ya kuwa utaratibu uliotolewa na Bodi ya Amani ya Rais wa Marekani Donald Trump Julai 31 kutoa wito kwa Hamas kusalimisha silaha na Israel kuondoka eneo hilo kufanyike taratibu na sanjari.
‘Juhudi zetu’
Kuangazia suala zima la mzozo katika kanda, Ansari alisema juhudi za sasa hivi za Qatar zinaangazia kumaliza hali tete na kuanza tena majadiliano ya Marekani na Iran.
“Kufikia sasa, juhudi zetu zinaangazia kusitisha uhasama na kuleta pande zote mbili kwenye mzozo huu pamoja kwa ajili ya majadiliano,” alisema.
Aliongeza kuwa Qatar inataka kuwepo kwa makubaliano kuhusu kufunguliwa tena kwa Mlangobahari wa Hormuz na kusitishwa mapigano kufikiwe pamoja.
Kuhusu marubani wa Iran walioingia anga ya Qatar, Ansari anasema Qatar ilipata maiti ya mmoja wa marubani hao wawili Machi 19 na baadaye kuikabidhi kwa Iran.
Alisema Iran haijajibu pendekezo la Qatar la kutaka itume wataalamu kufuatilia shughuli ya utafutaji.















