Mkataba wa Makkah unakaribisha mataifa mengine rafiki: Erdogan wa Uturuki

Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, amesema kuwa Mkataba wa Makkah wa Ulinzi wa Pamoja utaimarisha ushirikiano katika masuala ya usalama na ulinzi, miradi ya pamoja ya sekta ya ulinzi, pamoja na juhudi za kupambana na ugaidi.

Newstimehub

Newstimehub

7 Agosti, 2026

9dca57df e59a 4e90 b289 bb00c3f9868e 1786119428396

Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, amesema kuwa Makubalino ya Pamoja wa Ulinzi uliotiwa saini kati ya Uturuki, Saudi Arabia na Pakistan haulengi nchi yoyote, na uko wazi kwa ushiriki wa mataifa mengine rafiki yanayotafuta amani, ustawi na utulivu katika eneo hili.

Katika ujumbe aliouchapisha Ijumaa kwenye mtandao wa kijamii wa Uturuki wa NSosyal, Erdogan amesema kuwa mkataba huo, unaojengwa juu ya kanuni ya kuzuia uchokozi kwa nguvu ya pamoja dhidi ya vitisho, utaimarisha ushirikiano wa usalama na ulinzi, miradi ya pamoja ya sekta ya ulinzi na juhudi za kupambana na ugaidi.

Amesema pia kuwa mkataba huo unathibitisha tena haki ya kujilinda kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 51 ya Umoja wa Mataifa.

“Mkataba huu haulengi nchi yoyote bali uko wazi kwa mataifa rafiki yanayotafuta amani, ustawi na utulivu katika eneo letu,” amesema Erdogan.

Ameongeza kuwa Uturuki itaendelea kushikilia msimamo wake wa msingi wa kutatua migogoro na misukosuko kupitia mazungumzo na diplomasia, kwa kuheshimu sheria za kimataifa na kwa kuzingatia maono yake ya umiliki wa kikanda, ambapo mataifa ya eneo husika huongoza na kubeba jukumu la kutafuta suluhu za changamoto zinazowakabili.

Erdogan amesema amesafiri kwenda Makkah mapema Ijumaa kwa mwaliko wa Mwanamfalme na Waziri Mkuu wa Saudi Arabia, Mohammed bin Salman, ambako alikutana naye pamoja na Waziri Mkuu wa Pakistan, Shehbaz Sharif.

“Katika mkutano huo, sisi kama nchi tatu tulitia saini Mkataba wa Pamoja wa Ulinzi,” amesema.

Erdogan ameeleza matumaini yake kuwa ziara hiyo, mashauriano yaliyofanyika na mkataba huo yatakuwa na manufaa kwa eneo zima.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kutoka kwa maafisa wa Uturuki, mkataba huo ni makubaliano ya ushirikiano wa kiulinzi ambayo hayalengi nchi yoyote, na yameundwa kuimarisha dhamira ya kudumisha amani, utulivu na ustawi wa kikanda na kimataifa kupitia mgawanyo wa majukumu na mtazamo wa pamoja wa usalama.

Maafisa hao wameongeza kuwa mkataba huo unalenga kuimarisha uwezo wa pamoja wa kuzuia vitendo vya uchokozi, na unaeleza kwamba shambulio la silaha dhidi ya mojawapo ya nchi hizo tatu litachukuliwa kuwa ni shambulio dhidi ya nchi hizo zote.

Aidha, waliueleza mkataba huo kuwa ni matokeo halisi ya juhudi za muda mrefu za kidiplomasia zilizotekelezwa kwa kuzingatia kanuni ya umiliki wa kikanda, kwa lengo la kuweka mfumo wa pamoja wa kukabiliana na ongezeko la vitisho vya usalama wa kikanda na kimataifa.

Maafisa hao pia wamesema kuwa mkataba huo unatoa nafasi ya kupanua ushirikiano katika sekta ya ulinzi, ikiwemo ushirikiano wa viwanda vya ulinzi na kuimarisha uwezo wa majeshi ya nchi hizo kufanya kazi kwa pamoja.