Kiongozi wa upinzani Zambia ahitajika polisi kwa mahojiano

Mundubile na Zulu wamekanusha madai ya polisi kwamba muungano wao ulihusika katika uasi au shughuli za wanamgambo.

Newstimehub

Newstimehub

21 Agosti, 2026

4d84e4ae 4b98 4ac1 854b e3a5e82708bc 1787315412716

Jeshi la Polisi la Zambia limemuita kiongozi wa upinzani nchini humo, Brian Mundubile kwa ajili ya mahojiano, kwa kudaiwa kuhatarisha usalama wa taifa.

Taarifa ya polisi ilisema imekuwa ikifanya uchunguzi kwa miaka kadhaa kuhusu “vitisho vikubwa kwa usalama wa taifa” na ilitaka kumhoji Mundubile pamoja na mgombea mwenza wake, Makebi Zulu, ili kuweza kujiridhisha na uchunguzi wao.

Hata hivyo, jeshi hilo halikuweka bayana, vitisho hivyo vinahusu nini, japo walisisitizia “shughuli za kutia shaka” ambazo zilikuwa na uwezo wa kuhatarisha usalama wa taifa, kama zilivyoripotiwa katika maeneo yanayohusishwa na wawili hao.

Mundubile na Zulu wamekanusha madai ya polisi kwamba muungano wao ulihusika katika uasi au shughuli za wanamgambo.

Mundubile amekimbilia mafichoni wiki iliyopita akiwa chini ya hifadhi ya shirika la kimataifa la haki za binadamu, baada ya polisi kuvamia nyumba yake katika mji mkuu, Lusaka.

Aliyekuwa waziri wa baraza la mawaziri, Mutotwe Kafwaya, alipigwa risasi na kuuawa wakati wa operesheni ya Agosti 14, ambapo watu 11, wakiwemo viongozi muhimu wa upinzani, walikamatwa kwa tuhuma za makosa yanayohusiana na uhaini.

Siku ya Alhamisi, maafisa wa uhamiaji walisema wamemkamata katibu mkuu wa muungano wa upinzani.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, serikali imehakikishia shirika linalowahifadhi viongozi hao wawili kwamba “hakuna madhara yoyote yanayokusudiwa dhidi yao kwa namna yoyote ile.”

Ingawa uchaguzi wa wiki iliyopita ulikuwa wa amani kwa kiasi kikubwa, waangalizi wa kimataifa walisema mchakato huo ulikumbwa na madai kutoka kwa upinzani kuhusu vitisho, kukamtwa kwa watu, utekaji na vitendo vya vurugu.