Ghana yasherehekea mwisho wa utumwa kwa wito wa fidia

Nchi hiyo ya Afrika Magharibi inapanga hatua zinazofuata baada ya azimio la kihistoria la Umoja wa Mataifa kutangaza biashara ya utumwa katika Bahari ya Atlantiki kuwa uhalifu mkubwa dhidi ya ubinadamu.

Newstimehub

Newstimehub

21 Juni, 2026

2026 06 19t193945z 1174811317 rc2zwlazswly rtrmadp 3 ghana slavery

Taswira ya wanaume na wanawake, nusu uchi huku wamefungwa pingu na vilio vyao vya kuhuzunisha vilivyosikika katika Kasri la Christiansborg la Ghana kulifanya baadhi ya vizazi vya Waafrika waliokuwa watumwa kutiririkwa machozi siku ya Ijumaa, wakati wa kile nchi hiyo ya Afrika Magharibi inasema ni ukumbusho wa kwanza wa Juneteenth, uliofanyika nje ya Marekani.

Onyesho la kuigiza watumwa wakitayarishwa kwa safari ya meli ya mwisho kutoka Ghana kuvuka Bahari ya Atlantiki, lilikuwa hitimisho la kongamano la siku tatu lililoandaliwa na Ghana kuainisha hatua zinazofuata baada ya azimio muhimu la Umoja wa Mataifa kutangaza biashara ya utumwa katika Bahari ya Atlantiki kuwa uhalifu mkubwa dhidi ya binadamu.

“Kuona watoto wachanga na watoto wadogo (wanaoshikiliwa na akina mama waliofungwa pingu), ilikuwa yakudhihirisha uhalisia sana kwangu,” alisema Gaynel Diana Curry, ambaye anatoka Bahamas na anayeshikili uenyekiti wa Jukwaa la Kudumu la Umoja wa Mataifa la Watu Wenye Asili ya Afrika.

“Na kusikia kilio na kuona mashimo ya watumwa ilinigusa sana,” alisema Curry, ambaye alitembelea ngome hiyo hapo awali.

Akiwa amesimama kando yake, mwanamke mwingine, aliyesema kwamba anatoka Uingereza, alibubujikwa na machozi.

Verene Shepherd, msomi wa Jamaika na profesa wa historia ya kijamii, alisema kwamba ingawa mauigizo yanaweza kuonekana kama burudani kwa wengine, “kwa sisi ambao ni vizazi vyao, huu ni uchungu wetu unaoonyeshwa”.

Haki ya fidia

Mkutano huo nchini Ghana ulitafuta hatua madhubuti ikiwa ni pamoja na haki ya ulipaji fidia baada ya azimio la Umoja wa Mataifa.

“Tunachosema katika harakati za fidia ni kwamba haikuwa sawa kufanya hivi kwa watu, kwa wanadamu, iwe weusi , weupe, au chochote,” alisema Shepherd.

Kwa Waziri Mkuu wa Barbados Mia Mottley, ambaye ametembelea kasri hilo hapo awali, “hakuna kilichomtayarisha” kwa onyesho hilo. Ilikuwa “ukweli wa ujasiri wa ukandamizaji”.

Ikiwa na makumi ya ngome na majumba, Ghana ina idadi kubwa zaidi wa ngome za biashara ambazo zilitumika kwa usafirishaji wa watumwa kutoka Afrika.

Tarehe 19 Juni ni sikukuu ya shirikisho la Marekani inayojulikana kama “Juneteenth”, ambayo huadhimisha mwisho wa utumwa.

Rais wa Ghana John Mahama alisema ukumbusho wa Junetheenth huko Accra ulisherehekea kizazi cha watumwa nchini Marekani “kwa ujasiri wao, kwa ajili ya kuishi, kwa nguvu zao”.

‘Kurejesha heshima’

Mkutano huo ulioandaliwa na Ghana ulikuja na waraka wa kurasa 10 wenye maamuzi “yanayofikia mbali”, kulingana na waziri wa mambo ya nje wa Ghana Sam Okudzeto Ablakwa.

Hati hiyo iliorodhesha kati ya maamuzi mengine wito “wa uhamasishaji wa rasilimali za kutosha na endelevu za kifedha na kiufundi, ikijumuisha kupitia ushirikiano wa kimataifa na mbinu bunifu za ufadhili ili kusaidia juhudi na mipango ya fidia”.

Serikali ya Uholanzi iliwasilisha katika mkutano orodha ya vitu 2,000 vya sanaa ambayo inapanga kurejea Ghana.