Uturuki yataka Tunisia kumuachia kiongozi wa chama cha Ennahda

Spika wa Bunge la Uturuki, Numan Kurtulmus, amesema Rached Ghannouchi anahitaji matibabu kufuatia umri wake na hali yake ya afya.

Newstimehub

Newstimehub

13 Agosti, 2026

5c1d4083 5f1d 454b 96a3 7672bcacdff4 1786624390307

Spika wa Bunge la Uturuki, Numan Kurtulmus, siku ya Alhamisi ametoa wito kwa kiongozi wa Harakati ya Ennahda na Spika wa zamani wa Bunge la Tunisia, Rached Ghannouchi, ambaye yuko gerezani, kupewa matibabu na kuachiwa kwa kuzingatiwa utu na ubinadamu.

Kurtulmus amesema kupitia NSosyal, mtandao wa kijamii wa Uturuki, kwamba anafuatilia kwa karibu hali ya Ghannouchi, ambaye amemtaja kuwa “miongoni mwa watu mashuhuri katika mapambano ya amani, demokrasia na mshikamano.”

Amongeza kuwa Ghannouchi amesitisha kugoma kula na kutumia dawa, baada ya kuombwa kufanya hivyo na madaktari wanaofuatilia hali yake.

“Kwa kuzingatia umri wake mkubwa na matatizo ya kiafya aliyonayo, uzito wa hali ya Ghannouchi haupaswi kupuuzwa,” alisema Kurtulmus.

Amemtaja Ghannouchi kuwa mtu aliyejitolea maisha yake kwa “mustakabali wa watu wa Tunisia, uhuru, haki na demokrasia,” akisema licha ya shinikizo, na kuishi uhamishoni na kufungwa, hakuachana na “maadili aliyoyaamini na mapambano yake ya kidemokrasia.”

Kurtulmus amesema Ghannouchi amepata kutambuliwa kwa kiwango kikubwa nchini Tunisia na kimataifa kutokana na “msimamo wake wa kidemokrasia wakati wa kipindi cha mpito, msingi wake imara wa kielimu na mawazo yake.”

“Kwa kuakisi uhusiano wa kina wa kindugu uliopo kati ya watu wa Uturuki na Tunisia, namuombea afya njema na natumaini kwamba atarejea katika hali nzuri ya kiafya haraka iwezekanavyo,” alisema.

“Jambo tunalolitamani zaidi ni kwamba apewe kikamilifu msaada wa matibabu unaohitajika, apewe mazingira ya haki na ya kibinadamu yanayohitajika kwa ajili ya kuheshimu utu wa binadamu, na aachiliwe.”

Kuzuiliwa kwa Ghannouchi

Ghannouchi, ambaye alikuwa Spika wa Bunge lililovunjwa na Rais Kais Saied, amekuwa gerezani tangu alipokamatwa Aprili 17, 2023.

Mahakama iliamuru azuiliwe katika kesi iliyohusiana na matamshi yaliyodaiwa kutolewa na yeye, akishtakiwa kwa “kuchochea dhidi ya usalama wa taifa.” Baadaye alihukumiwa kifungo chaa gerezani katika kesi kadhaa, lakini ameyakataa mashtaka hayo na kusema kuwa yana msukumo wa kisiasa.