Shirika la kijasusi la Afrika Kusini lilisema siku ya Jumatatu kuwa zaidi ya watu 25,000 wamerejeshwa makwao katika wiki za hivi karibuni kabla ya maandamano ya kupinga wahamiaji yaliyopangwa, na wengine wengi bado wanasubiri kuondoka.
Uhamaji huo unakuja huku maelfu wakitafuta kuondoka kwa hofu ya usalama baada ya makundi yanayoongozwa na raia kutoa makataa yasiyo rasmi kwa wageni wasio na vibali kuondoka nchini ifikapo Juni 30.
Serikali kadhaa, ikiwa ni pamoja na Nigeria, Malawi, Ghana, Zimbabwe na Msumbiji, zimeandaa safari za ndege na mabasi kwa hiari baada ya wiki kadhaa za maandamano yaliyolenga wageni.
“Kufikia sasa, zaidi ya raia 25,000 wa kigeni wamerejeshwa makwao,” Muundo wa Kitaifa wa Uendeshaji na Ujasusi (NATJOINTS), ambao unaratibu shughuli za usalama zinazohusishwa na maandamano hayo, ulisema.
‘Mchakato unaoendelea’
Takwimu za hivi punde zinaashiria ongezeko kubwa kutoka wiki iliyopita, wakati mamlaka iliposema Wamalawi 15,000 walikuwa wamepangiwa kuondoka. Takriban Waghana 988 na takriban Wanigeria 600 waliondoka kwa ndege mapema mwezi huu.
“Huu ni mchakato unaoendelea,” NATJOINTS ilisema, na kuongeza kuwa vitengo maalum, ikiwa ni pamoja na timu za K9 na kitengo cha wana anga , vimetumwa.
Vikundi vinavyopinga uhamiaji haramu vimeunga mkono makataa ya Jumanne ambayo hayajaidhinishwa, na kuwataka wahamiaji wasio na vibali kuondoka la sivyo watakabiliwa na madhara.
Wameandaa mfululizo wa maandamano kote nchini.
Muethiopia, Msumbiji, Mmalawi miongoni mwa waliofariki
Makundi ya watu kwa wakati huo yameenda nyumba hadi nyumba kuwaambia wahamiaji kuondoka au kuwataka kuonyesha hati zao.
“Hisia dhidi ya wageni” imewaacha watu wanne wakiwa wamekufa, NATJOINTS ilisema.
Polisi waliiambia AFP kuwa waathiriwa ni pamoja na raia wawili wa Msumbiji, Muethiopia na Mmalawi.
Kuongezeka kwa hofu ya usalama kumesababisha maelfu ya wahamiaji kukusanyika kwa muda kusini mashariki mwa Durban, kitovu cha watalii cha Cape Town, na mji mkuu wa kifedha wa Johannesburg wakisubiri usafiri hadi nchi zao.
Ukosefu wa ajira
Afrika Kusini, kivutio cha muda mrefu cha ajira ya wahamiaji, inakabiliana na ukosefu wa ajira zaidi ya 30% na historia ya machafuko ya mara kwa mara dhidi ya wageni, ambayo mara nyingi yanachochewa na madai kwamba wahamiaji huchukua kazi.
Machafuko ya siku za nyuma yanayowalenga raia wa kigeni wasio na vibali yamesababisha vifo, huku watu 62 wakiuawa katika ghasia mwaka 2008.















