Hichilema ashinda Uchaguzi wa Zambia

Ushindi huo umemuwezesha Hichilema kuvuka kizingiti cha kikatiba cha kupata zaidi ya asilimia 50.

Newstimehub

Newstimehub

18 Agosti, 2026

75d3cf87 336d 4241 a4db 6c5229eb4cd5 1787036433868

Hakainde Hichilema ameshinda katika Uchaguzi Mkuu wa urais nchini Zambia baada ya kumshinda mpinzani wake wa karibu, Brian Mundubile, kwa zaidi ya kura milioni 1.1.

Hakainde Hichilema, amepata zaidi ya kura milioni 2.9 na hivyo kujihakikishia nafasi ya kuliongoza taifa hilo kwa muhula wa pili. Matokeo hayo ni kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi ya Zambia.

Brian Mundubile mpinzani kutoka Chama cha National Restoration Party for Unity and Progress (NRPUP), amepata kura milioni 1.8.

Ushindi huo umemuwezesha Hichilema kuvuka kizingiti cha kikatiba cha kupata zaidi ya asilimia 50.

“Tunawashukuru Wazambia. Kwa kweli tumeheshimiwa na kuaminiwa kwa kutukabidhi dhamana ya kuongoza ofisi ya juu kabisa ya nchi yetu na kuturuhusu kuwa watumishi wenu tena,” Hichilema amesema katika ujumbe aliouweka katika mtandao wa kijamii wa Facebook muda mfupi baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zambia, Mwanagala Zaloumis, kumtangaza kuwa rais mteule katika kituo cha kitaifa cha kutangazia matokeo jijini Lusaka, mji mkuu wa Zambia.

Zaloumis amesema Hichilema ameshinda kwa kiwango kikubwa kiasi kwamba matokeo kutoka katika vituo maalumu vya kupigia kura vilivyosalia katika majimbo bunge matano kati ya majimbo bunge 226 ya nchi hiyo hayawezi kubadili kwa kiwango cha maana matokeo ya uchaguzi.

Mitaa ya Lusaka ilikuwa tayari imechangamka kabla hata ya kutangazwa rasmi kwa ushindi wa Hichilema, na iliendelea kuwa na shamrashamra kwa muda mrefu baadaye. Watu kutoka makundi mbalimbali ya jamii walijaa mitaani, wakivumilia hali ya hewa baridi mapema asubuhi kusherehekea ushindi huo.

“Mheshimiwa Rais, tafadhali endelea kuwa kiongozi mzuri kwa nchi hii. Watu wa Zambia wameonyesha tena imani na matumaini yao katika uongozi wako,” amesema Collins Maoma, Mwenyekiti wa Kitaifa wa chama kilichomsimamisha Hichilema, chama tawala cha United Party for National Development (UPND), alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.