Sudan imeandaa sherehe rasmi siku ya Jumanne, 13 Januari, huko Port Sudan kutangaza urejeshwaji wa vito 570 vya kale vya Sudan vilivyoibwa wakati wa mgogoro unaoendelea nchini.
Katika mwaliko rasmi, Waziri wa Utamaduni, Habari na Utalii Khalid Al-Eisir alitangaza kuwa serikali itafungua rasmi vito vilivyorejeshwa, ambavyo vinashughulikia nyakati nyingi kihistoria, kuanzia zama za historia ya kale hadi enzi za kisasa.
Waziri Al-Eisir alielezea urejeshwaji wa vito hivi vya kale kama mafanikio makubwa ya kitaifa, akisema unaonyesha azma ya serikali ya kulinda urithi wa ustaarabu wa Sudan na kudai tena mali yake ya kitamaduni, ripoti za vyombo vya habari vya serikali SUNA zinaonyesha.
Makumbusho ya Sudan yaliibiwa kwa wingi siku za mwanzo za vita kati ya jeshi la Sudan na Jeshi la Msaada la Haraka (Rapid Support Forces) mwezi Aprili 2023. Maelfu ya vito vya thamani kubwa, vingi vyao vinatoka katika Ufalme wa Kush wa miaka karibu 3,000 iliyopita, vilitoweka wakati wa vurugu hizo.
Vito vilivyoibiwa
Kwa mujibu wa maafisa, zaidi ya makumbusho 20 nchini kote yaliibiwa au yaliharibiwa, na hasara zinazokadiriwa zilifikia takriban dola za Kimarekani milioni 110.
Maeneo yaliolengwa wakati wa mapigano yalihusisha Makumbusho ya Ikulu ya Rais, Makumbusho ya Vikosi vya Ulinzi, Makumbusho ya Nyumba ya Khalifa, Makumbusho ya Etnografia, na Makumbusho ya Historia ya Asili katika Chuo Kikuu cha Khartoum.
Mamlaka zilisema awali kuwa baadhi ya vitu vilivyoibwa tayari vilivukishwa mipaka kimagendo na sehemu kubwa ya vito hivyo bado havijulikani vilipo.
Hata hivyo, tangu Aprili 2025, serikali ya Sudan imekuwa ikifanya kazi na Interpol na UNESCO kurejesha mali za kitamaduni zilizochukuliwa ambazo inadhaniwa kuhamishwa hadi nchi jirani. Mnamo Septemba mwaka uliopita, UNESCO ilitoa tahadhari ya kimataifa ikiwaonya majumba ya makumbusho, wakusanyaji, na nyumba za mnada wasichukue au kuwezesha biashara ya mali ya kitamaduni inayotoka Sudan.









