Jeshi la Sudan lachukua udhibiti wa maeneo muhimu kutoka kwa RSF karibu na mpaka wa Ethiopia

Jeshi linasema kuwa vikosi vyake vimechukua tena udhibiti wa eneo la Al-Silk katika jimbo la Blue Nile

Newstimehub

Newstimehub

26 Januari, 2026

a74b0174fc2cf4140c718c404fa8989521399f54e04e2dca0d4751311551f2b2

Jeshi la Sudan limechukuwa tena udhibiti wa eneo la Al-Silk katika jimbo la Blue Nile karibu na mpaka wa Ethiopia kutoka kwa wapiganaji wa Rapid Support Forces (RSF), jeshi lilisema siku ya Jumatatu.

Katika taarifa, jeshi lilisema kuwa kamandi yake ya 4 ilichukua udhibiti wa eneo hilo “baada ya operesheni iliyokuwa imepangwa vizuri iliyosababisha kuondolewa kwa wapiganaji wa RSF.”

Taarifa hiyo ilisema makabiliano hayo yalisababisha athari kubwa kwa RSF na washirika wake, Sudan People’s Liberation Movement-North (SPLM-N).

Hakukuwa na taarifa yoyote kutoka kwa kundi hilo la waasi.

Siku ya Jumapili, jeshi lilitibua mashambulizi yaliyoanzishwa na RSF katika eneo la Al-Silk na Malkan jimbo la Blue Nile.

Awali vyanzo vya kijeshi viliiambia Anadolu kuwa vikosi vya jeshi viliwatimua RSF na SPLM nje ya mji wa Habila huko Kordofan Kusini.

Vita kati ya jeshi la Sudan na RSF, vilivyoanza Aprili 2023, vimewaua maelfu ya watu na kuwaacha mamilioni wengine bila makazi.