Hakutakuwa na amani nchini Sudan hadi kuondolewa kwa wanamgambo wa RSF, alisema Abdel Fattah al-Burhan, Mkuu wa jeshi wa nchi hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari katika makazi yake mjini Port Sudan siku ya Jumapili, Burhan alisema: “Hakutakuwa na amani hadi RSF iondolewe, na pendekezo lolote la suluhu linaloihusisha RSF si chochote ila kuahirisha mgogoro. Suluhu ya kudumu ni kuiondoa RSF. Hii haimaanishi kwamba wote lazima wafe; inaweza pia kumaanisha kuweka chini silaha na kujisalimisha.”
Burhan alisisitiza kuwa mgogoro huo umesababisha uharibifu mkubwa, vifo vingi vya raia na hasara kubwa ya mali kote nchini. Aliongeza kuwa hakuna raia wa Sudan ambaye hajaathiriwa na vita hivyo, na kwamba wananchi bado wamesimama kwa umoja dhidi ya kundi hilo la waasi.
Akizungumzia juhudi za kimataifa za kusitisha mapigano, alisema kumekuwa na ongezeko la wito wa kusitisha vita baada ya kuanguka kwa mji wa Al Fasher mwezi Oktoba, akidai kuwa wito huo uliambatana na majaribio ya kuruhusu RSF kupanua udhibiti wake wa maeneo.
“Hakukuwa na mapendekezo ya kusitisha mapigano wakati wa kuzingirwa kwa Al Fasher,” alisema. “Baada ya mji huo kuanguka, wito ukaongezeka kwa sababu wanataka RSF idhibiti maeneo zaidi.”
RSF yakataa wapatanishi
Burhan alisema Sudan ilipendekeza Uturuki au Qatar kuwa wapatanishi, lakini RSF ilikataa pendekezo hilo. Aliongeza kuwa nchi za kikanda kama Saudi Arabia na Misri pia zinaweza kushiriki katika juhudi za upatanishi.
“Tunamwamini Mungu kwanza, kisha (Rais wa Uturuki Recep Tayyip) Erdogan,” alisema.
Pia alisisitiza kuwa RSF na jeshi la Sudan si nguvu zilizo sawa. “Pande mbili zinazopigana hapa si sawa. RSF si sawa na jeshi la Sudan. Dunia nzima inasema hivyo,” alisema.
Licha ya maazimio ya Umoja wa Mataifa, Burhan alisema RSF inaendelea kufanya mashambulizi na kusafirisha silaha kupitia njia ya magendo kuingia Sudan, hasa katika eneo la Darfur, bila kuchukuliwa hatua madhubuti.
“Sisi, kama watu wa Sudan na jeshi, tumeazimia kuiondoa RSF,” alisema. “Tuko tayari kwa suluhu zote za amani.”
Sudan imekumbwa na mapigano tangu Aprili 2023 kati ya jeshi la Sudan na RSF kufuatia mivutano kuhusu kuunganisha jeshi na wanamgambo wa RSF.
Mgogoro huo umesababisha moja ya majanga mabaya zaidi ya kibinadamu duniani, ambapo makumi ya maelfu wameuawa na mamilioni wamekimbia makazi yao.














